Yaliyomo | Sura Iliyopita | Sura Ifuatayo | Mwisho wa Ukurasa | Pa Kuanzia
Unaruhusiwa kuchapa, kunakili, kugawa au kusambaza haya kwa njia yoyote ile, mradi tu usibadili chochote wala kukata chochote. Vile vile hairuhusiwi kuuza maelezo haya. © Haki zote zimehifadhiwa David Servant
SURA YA SITA
Mahubiri Makuu Ya Yesu Kuhusu Wokovu, 1
Miaka elfu mbili iliyopita, Mwana wa Mungu akiwa anaishi duniani katika mwili wa mwanadamu alizungumza na kundi la watu waliokuwa wamekusanyika kumsikiliza pembeni ya kilima karibu na Bahari ya Galilaya. Siku hizi maneno Yake hayo tunayaita “Mahubiri ya Mlimani”.
Yesu alikuwa bingwa wa mawasiliano kuliko wote waliowahi kuwepo, Naye alikuwa anawafundisha watu ambao tunaweza kuwahesabu kuwa wenyeji ambao hawakuwa na elimu. Kwa hiyo, mafundisho Yake yalikuwa rahisi tu kuelewa. Alitumia vitu vya kila siku ili kufafanua hoja Zake. Lakini siku hizi kuna wengi wanaofikiri kwamba unahitaji mtu mwenye digrii ya Udaktari wa Falsafa (PhD) ili kuweza kutafsiri yale aliyosema Yesu. Na bahati mbaya kabisa ni kwamba, baadhi ya hao watafsiri wanasema kwamba Yesu hakumaanisha alichosema. Basi, wameunda nadharia nyingi za ajabu ili kujaribu kueleza kile ambacho Yesu alisema kweli, na nadharia hizo zisingeweza kueleweka na wale watu wa kawaida ambao Yesu alisema nao hata kwa miaka elfu nzima, wala wasingeweza kuelewa nadharia hizo kama zingefafanuliwa. Kwa mfano: Kuna “wataalamu wa Biblia” wa kisasa wanaotaka tuamini kwamba maneno ya Yesu hayakuwa yanawahusu wasikilizaji Wake wala Wakristo wa siku hizi, bali yatafanya kazi wakati tutakapokuwa tunaishi katika ufalme Wake wa milele! Nadharia ya ajabu hiyo, ukizingatia ukweli kwamba wakati Yesu alipokuwa anazungumza na wasikilizaji Wake alitumia neno ninyi (sio wao) zaidi ya mara mia moja katika mahubiri hayo mafupi. Hawa “wasomi wa Biblia” wanamfanya Yesu kuwa mwongo.
Naomba pia nionyeshe kwamba mahubiri ya Yesu yalikuwa yamelengwa kwa watu wengi waliokuwa wamekusanyika ili kumsikiliza, si kwa wanafunzi Wake tu (ona Mathayo 7:28). Na yalikuwa yanawahusu wanadamu wote tangu wakati ule, ikiwa tutasoma mahubiri hayo kwa udhati wa moyo.
Kusudi la sura hii na ijayo ni kujifunza Mahubiri ya Mlimani ya Yesu. Tutakapofanya hivyo, tutagundua kwamba yalikuwa mahubiri kuhusu wokovu, utakatifu na mahusiano kati ya hivyo viwili. Ni mahubiri yenye kutoa maonyo mara kadhaa kuhusu hatari ya kutoshika sheria. Akiwa anawajali sana wale watu maskini lakini wenye njaa ya kiroho ambao walikusanyika kumsikiliza, Yesu alitaka waelewe kilicho muhimu zaidi – jinsi ambavyo wangeweza kurithi ufalme wa mbinguni. Ni muhimu kwamba hata sisi tujali kile alichosema. Huyu ndiye aliyeandikiwa na Musa, hivi: “Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii katika ndugu zenu, kama mimi; msikieni yeye katika mambo yote atakayonena nanyi. Na itakuwa ya kwamba kila mtu asiyemsikiliza nabii huyo ataangamizwa na kutengwa na watu wake” (Matendo 3:22-23). Acha tuanzie mwanzo.
Wenye Heri
Katika sehemu ya kwanza ya mahubiri ya Yesu – sehemu ya “heri” – aliahidi baraka maalum kwa watu wenye kuwa na tabia au hali fulani. Zipo tabia mbalimbali zinazotajwa na baraka nyingi kuahidiwa. Wasomao kwa haraka haraka mara nyingi husoma sehemu hii kama watu wanavyotazama utabiri wa nyota zao, wakifikiri kwamba kila mtu anapaswa kujikuta kwenye moja tu. Tunaposoma kwa makini zadi, tunatambua kwamba Yesu hakuwa anaorodhesha aina tofauti za watu watakaopata baraka mbalimbali, bali alikuwa anaorodhesha mtu aina moja atakayepokea baraka moja ya jumla: kuurithi ufalme wa Mungu. Hakuna njia nyingine ya kufafanua hicho vizuri.
Tuone basi mistari kumi na mbili ya kwanza ya Mahubiri ya Mlimani.
“Naye alipowaona makutano, alipanda mlimani; na alipokwisha kuketi, wanafunzi wake walimjia. Akafumbua kinywa chake akawafundisha akisema,
‘Heri walio maskini wa roho; maana ufalme wa mbinguni ni wao.
‘Heri wenye huzuni; maana hao watafarijika.
‘Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.
‘Heri wenye njaa na kiu ya haki; maana hao watashibishwa.
‘Heri wenye rehema; maana hao watapata rehema.
‘Heri wenye moyo safi; maana hao watamwona Mungu.
‘Heri wapatanishi; maana hao wataitwa wana wa Mungu.
‘Heri wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki; maana ufalme wa mbinguni ni wao.
‘Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu’.” (Mathayo 5:1-12).
Baraka Zenyewe Na Hali-Tabia
Kwanza, hebu fikiri juu ya baraka zote zilizoahidiwa. Waliobarikiwa (au wenye heri) (1) wataurithi ufalme wa mbinguni, (2) watafarijiwa, (3) watairithi nchi, (4) watatoshelezwa katika haki, (5) watapata rehema, (6) watamwona Mungu, (7) wataitwa wana wa Mungu, (8) wataurithi ufalme wa mbinguni (ni marudio ya namba 1,) mahali ambapo watapewa thawabu.
Sasa basi: Yesu anataka sisi tufikiri kwamba ni wale walio maskini wa roho tu na wale ambao wameteswa kwa ajili ya haki ndiyo watakaorithi ufalme wa Mungu? Je, ni wale walio safi tu moyoni ndiyo watakaomwona Mungu na ni wapatanishi tu ndiyo watakaoitwa wana wa Mungu lakini hawatarithi ufalme wa Mungu? Je, wapatanishi hawatapokea rehema, na wenye rehema hawataitwa wana wa Mungu? Bila shaka sivyo Yesu anavyotaka tufikiri.
Sasa hebu fikiri zile halitabia tofauti ambazo Yesu anazitaja: (1) maskini wa roho, (2) mwenye huzuni, (3) mpole, (4) mwenye njaa na kiu ya haki, (5) mwenye rehema, (6) mwenye moyo safi, (7) mpatanishi, na (8) mwenye kuudhiwa au kuteswa.
Je, Yesu anataka tufikiri kwamba mtu anaweza kuwa msafi wa moyo na asiwe na rehema? Je, mtu anaweza kuteswa kwa ajili ya haki na asiwe mwenye njaa na kiu ya haki? Tunasema tena, si hivyo.
Basi, ni salama kabisa kufikiri kwamba hizo baraka nyingi zinazoahidiwa hao ni vipengele vya baraka moja kubwa – kuurithi ufalme wa Mungu. Na halitabia nyingi za hao waliobarikiwa zinapatikana kwa wote walio heri.
Ni dhahiri kwamba mahubiri haya yanaeleza halitabia za wafuasi wa kweli wa Yesu, na kwa kuziorodhesha alikuwa anawatia moyo wafuasi Wake kwa ahadi za baraka nyingi za wokovu. Waliobarikiwa ni watu walio-okoka, kwa hiyo, Yesu alikuwa anaeleza halitabia za watu wanaokwenda mbinguni. Watu wasioingia katika maelezo hayo hawajabarikiwa na hawataurithi ufalme wa mbinguni. Basi ni sawa kwetu kujiuliza kama tunaingia katika maelezo ya Yesu. Haya ni mahubiri kuhusu wokovu, utakatifu na uhusiano uliopo kati ya hayo mawili.
Hali-Tabia Za Waliobarikiwa
Zile sifa nane ambazo Yesu anaziorodhesha za watu waliobarikiwa zinaweza kufafanuliwa au kutafsiriwa kwa njia inayoeleweka zaidi. Kwa mfano: Kuna uzuri gani kuwa “maskini wa roho”? Mimi nadhani kwamba Yesu alika anataja sifa ya kwanza ya lazima ambayo mtu lazima awe nayo kama ataokoka – yaani, atambue umaskini wake kiroho. Ni lazima mtu aone hitaji la Mwokozi kwanza kabla hajaokoka.
Hii sifa ya kwanza inaondoa hali ya kujitosheleza na wazo lolote la kustahili wokovu. Yule aliyebarikiwa kweli ni mwenye kutambua kwamba hana chochote cha kumpa Mungu, kwamba haki yake ni kama “matambara machafu.” Anajiona miongoni mwa wale ambao “wametengwa na Kristo, wametengwa na Israeli, wageni kwa maagano na ahadi, wasio na matumaini na bila Mungu duniani” (Waefeso 2:12).
Tena, Yesu hakutaka mtu yeyote afikiri kwamba kwa juhudi zake mwenyewe anaweza kufikia viwango vile ambavyo alikuwa anataka kuvitaja. Hapana. Watu hubarikiwa na Mungu kama watakuwa na sifa hizo zinazotajwa. Vyote vinatoka katika neema ya Mungu. Wenye heri ambao Yesu aliwazungumzia hapa wamebarikiwa, si kwa sababu ya kile kinachowangojea mbinguni tu, bali kwa sababu ya kazi ambayo Mungu ameifanya maishani mwao hapa duniani. Ninapoona sifa za kubarikiwa maishani mwangu zinatakiwa kunikumbusha kile ambacho Mungu amefanya ndani yangu kwa neema Yake, siyo kile ambacho mimi nimefanya.
Kama halitabia ya kwanza imeorodheshwa kwanza kwa sababu ndiyo ya kwanza ya lazima kwa wanaokwenda mbinguni, basi hata ya pili ina maana: “Heri wenye huzuni” (Mathayo 5:4). Je, Yesu hapa alikuwa anazungumzia toba ya kutoka moyoni na kujisikia hatia kwa sababu ya dhambi? Nafikiri hivyo, hasa kwa sababu Maandiko yanasema wazi kwamba huzuni ya kimungu husababisha toba ambayo ni muhimu na lazima kwa ajili ya wokovu (2Wakor. 7:10). Kama sivyo, basi pengine Yesu alikuwa anazungumzia huzuni ambayo Wakristo wote wa kweli wanayo wanapoendelea kukabiliana na dunia iliyo katika hali ya kumwasi Mungu anayewapenda. Paulo anaieleza hiyo kuwa ni “huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni [mwake]” (Warumi 9:2).
Halitabia ya tatu – upole – inaorodheshwa pia katika Maandiko kwamba ni tunda mojawapo la Roho (ona Wagalatia 5:22-23). Upole si sifa inayotokana na mtu. Wale ambao wamepokea neema ya Mungu na Roho Mtakatifu anakaa ndani yao pia wamebarikiwa kuwa wapole. “Wakristo” wakali na wakorofi, jihadharini. Hampo miongoni mwa watakaorithi nchi.
Kuwa Na Njaa Na Kiu Ya Haki
Sifa ya nne – kuwa na njaa na kiu kwa ajili ya haki – hueleza juu ya shauku ya ndani itokayo kwa Mungu ambayo kila mtu aliyezaliwa mara ya pili anakuwa nayo. Anatamani kuwa mtakatifu na mwenye kumpendeza kabisa Bwana wake.
Mara nyingi tunaposoma neno haki katika Maandiko tunalitafsiri kuwa ni “haki tunayohesabiwa na Kristo,” lakini hiyo si maana yake kila wakati. Mara nyingi maana yake ni, “hali ya kuishi sawa kulingana na kiwango cha Mungu.” Hiyo ndiyo maana ya Yesu hapa, kwa sababu hakuna sababu ya kuwa na njaa ili kupata haki tuliyokwisha hesabiwa huku ni yetu tayari. Wale ambao wamezaliwa kwa Roho wanatamani kuishi kwa haki, na hilo pia linatusaidia sisi kuelewa kwamba hakuna Mkristo wa kweli aliye mkamilifu. Vinginevyo asingetamani kitu alicho nacho tayari. Lakini, sisi tunaotamani tunajua kwamba tuta”toshelezwa” (Mathayo 5:6), uhakika kwamba Mungu kwa neema Yake ataikamilisha kazi aliyoianza ndani yetu (ona Wafilipi 1:6). Hii ndiyo faraja ya pekee tuliyo nayo katika hali yetu ya kutokamilika sasa, kitu ambacho kinaendelea kutusumbua. Tunaichukua dhambi ambayo bado imo ndani yetu. Ila – kwa upande mwingine – mahubiri hayo na heri hizo zenyewe zinathibitisha kwamba kila mtu anayekwenda mbinguni, aliyebarikiwa na Mungu, anao utakatifu kiasi fulani sasa hivi.
Sifa ya tano – rehema – pia ni kitu ambacho kila mtu aliyezaliwa upya anakuwa nacho kwa sababu ya kuwa na Mungu mwenye rehema akikaa ndani yake. Wale wasiokuwa na rehema hawajabarikiwa na Mungu, na wanadhihirisha kwamba si washiriki wa neema Yake. Mtume Yakobo anakubaliana na hayo anaposema: “Maana hukumu haina huruma kwake yeye asiyeona huruma” (Yakobo 2:13). Ukisimama mbele za Mungu na upokee hukumu isiyo na huruma, utakwenda mbinguni au jehanamu?
Sifa ya sita ya mwenye kwenda mbinguni ni usafi wa moyo. Tofauti na wengi wanaojiita Wakristo, wafuasi wa kweli wa Kristo si watakatifu kwa nje tu. Kwa neema ya Mungu, mioyo yao imefanywa kuwa safi. Kweli wanampenda Mungu kutoka mioyoni mwao, na inagusa makusudi yao na tafakari zao. Yesu aliahidi kwamba hao watamwona Mungu.
Tena narudia kuuliza: Je, tuamini kwamba kuna waamini wa kweli Wakristo ambao si wasafi moyoni ambao kwa sababu hiyo hawatamwona Mungu? Je, Mungu atawaambia, “Ingia mbinguni, lakini hutaniona kamwe”? Hapana. Bila shaka kila anayekwenda mbinguni kweli ana moyo safi.
Waliobarikiwa Kuwa Wapatanishi
Wapatanishi wanafuata katika orodha. Wao wataitwa wana wa Mungu. Hapa tena, Yesu bila shaka alikuwa anasema juu ya kila mfuasi wa kweli wa Kristo, kwa sababu kila amwaminiye Kristo ni mwana wa Mungu (ona Wagalatia 3:26).
Wale waliozaliwa kwa Roho ni wapatanishi kwa njia kama tatu hivi:
Kwanza: Wamejipatanisha na Mungu, ambaye hapo kwanza alikuwa adui yao.
Pili: Wanaishi kwa amani, kadiri iwezekanavyo na pasipo kumkosea Mungu, na watu wengine pia. Wao si wagomvi au watu wa fujo. Paulo aliandika kwamba watu wa aina hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu (ona Wagalatia 5:19-21). Waamini wa kweli watakwenda maili ya ziada kuepuka ugomvi na kutunza amani katika mahusiano yao. Hawadai kuwa na amani na Mungu huku wakiwa na tofauti na ndugu (ona Mathayo 5:23-24; 1Yohana 4:20).
Tatu: Kwa kuwaambia wengine Injili, wafuasi wa kweli wa Kristo pia huwasaidia wengine kuwa na amani na Mungu na wenzao.
Mwisho: Yesu alisema wamebarikiwa wale wanaoudhiwa (au kuteswa) kwa ajili ya haki. Bila shaka alikuwa anazungunza juu ya watu wanaoishi maisha ya haki. Hao ndiyo wanaoteswa na wasioamini. Hao ndiyo watu watakaorithi ufalme wa Mungu.
Je, Yesu alikuwa anazungumza kuhusu mateso aina gani? Kuuawa? Kuteswa kimwili? Hapana. Yeye alisemea kuudhiwa kwa kusemwa vibaya na kutukanwa kwa ajili Yake. Maana yake ni kwamba wakati mtu anapokuwa Mkristo wa kweli, ni kitu kinachojulikana kwa wasioamini, la sivyo wasioamini wasingemsema vibaya. Je, ni wangapi wanaojiita Wakristo ambao hawana tofauti na wasioamini kiasi cha kwamba hakuna asiyeamini hata mmoja anayesema kinyume chao? Hao si Wakristo wa kweli. Yesu alisema hivi: “Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo” (Luka 6:26). Wakati watu wote wanapokusema vizuri, hiyo ni ishara kwamba wewe ni mwamini bandia. Dunia inawachukia Wakristo wa kweli (ona pia Yohana 15:18-21; Wagalatia 4:29; 2Timo. 3:12; 1Yohana 3:13-14). Je, kuna yeyote anayekuchukia? Haya ni mahubiri kuhusu wokovu, utakatifu na mahusiano ya hayo mawili.
Chumvi Na Nuru
Katika mistari inayofuata, Yesu aliendelea kueleza kuhusu wafuasi Wake wa kweli - waliobarikiwa – akiwalinganisha na chumvi na nuru. Vyote hivyo viwili vina sifa zinazoweza kuonekana. Chumvi ina ladha na nuru huangaza. Kama haina ladha, si chumvi. Kama haiangazi, si nuru.
“Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni” (Mathayo 5:13-16).
Siku za Yesu chumvi ilitumiwa kwa sehemu kubwa kwa kuhifadhia nyama. Kama wafuasi watiifu wa Kristo, sisi ndiyo tunaohifadhi dunia hii isiharibike kabisa kabisa na kuoza. Lakini, kama na sisi tutakuwa kama dunia katika mwenendo wetu, kweli hatufai kwa lolote. Yesu aliwaonya wale waliobarikiwa wadumu kuwa na ladha, wakitunza upekee wao. Lazima wabakie tofauti na dunia inayowazunguka, wasije wakapoteza “ladha” na kustahili “kutupwa nje na kukanyagwa na watu”. Hili ni onyo mojawapo kati ya mengi kuhusu kurudi nyuma wanalopewa waamini wa kweli katika Agano Jipya. Kama chumvi ni chumvi kweli, inakuwa na ladha. Vivyo hivyo, wafuasi wa Yesu wanatenda kama wafuasi wa Yesu. La sivyo si wafuasi wa Yesu, hata kama walikuwa hapo kwanza.
Wafuasi wa kweli wa Kristo pia ni nuru ya dunia. Kila mara nuru huangaza. Kama haiangazi, basi si nuru. Katika mfano huu, nuru huwakilisha matendo yetu mema (Mathayo 5:16). Kristo aliwashauri wafuasi Wake kutenda matendo yao mema ili watu wengine wayaone. Kwa njia hiyo, watamtukuza Baba yao wa mbinguni kwa sababu Yeye ndiye chanzo cha kazi au matendo hayo mema.
Ona kwamba Yesu hakusema tutengeneze mwanga, bali tuache nuru tuliyo nayo iangaze mbele ya wengine ili watu waone mwanga wetu. Hakuwa anashauri wale wasiokuwa na matendo wafanye mpango wa kuyapata, bali aliwashauri wale wenye matendo mema wasiyafiche. Wafuasi wa Kristo ni nuru ya ulimwengu. Wamebarikiwa, kwa neema ya Mungu, kuwa mianga gizani.
Umuhimu Wa Kushika Amri Za Mungu
Hapo tunafikia mahali pa kuanza fungu lingine la maneno. Katika fungu hili, Yesu alianza kuzungumza kuhusu Torati na uhusiano wake kwa wafuasi Wake.
“Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua bali kutimiliza. Kwa maana, amin nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka, hata yote yatimie. Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni. Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni” (Mathayo 5:17-20).
Kama Yesu aliwaonya wasikilizaji Wake dhidi ya kufikiri kwamba alikuwa anaibatilisha Torati au hata Manabii, basi tunaweza kufikiri kwamba kuna waliokuwa wakimsikiliza waliodhani hivyo. Tunaweza kukisia kilichosababisha wafikiri hivyo. Pengine ni kule kukemea kwa ukali sana mambo ya Mafarisayo na waandishi.
Vyovyote vile, Yesu alitaka kila mtu ajue wakati ule na sasa kwamba kufikiri hivyo ni makosa. Yeye alikuwa Mungu – aliyevuvia Agano la Kale zima – kwa hiyo hakika asingeondoa kila kitu alichokuwa amesema kwa njia ya Musa na manabii. Kinyume chake, angeitimiza Torati na Manabii.
Je, angetimizaje Torati na Manabii? Wengine wanafikiri kwamba Yesu alikuwa anazungumzia tu kule kutimizwa kwa unabii wa Masiya. Ingawa kweli Yesu alitimiza (na atatimiza bado) kila utabiri wa Kimasiya, Yeye hakumaanisha hivyo. Mantiki inaonyesha kwamba alikuwa anazungumza juu ya yote yaliyoandikwa katika Torati na Manabii, mpaka “yodi na nukta ndogo sana” (ms. 18) ya Torati, na mpaka iliyo “ndogo” kabisa (ms. 19) katika amri (si utabiri wa Masiya tu).
Kuna wanaofikiri Yesu alimaanisha kwamba angeitimiza Torati kwa kutosheleza masharti yake kwa niaba yetu kupitia maisha Yake ya utii na kifo Chake cha kujitoa kama dhabihu. Lakini hilo nalo, kulingana na mantiki, silo alilokuwa akisema. Katika mistari inayofuata, Yesu hasemi chochote juu ya maisha au kifo Chake kwamba ndiyo kipimo cha kutimizwa Torati. Badala yake, katika sentensi inayofuata, anataja kwamba Torati itaendelea kufanya kazi mpaka “mbingu na nchi” zitakapopita” na kila kitu “kitimizwe”. Kisha anataja kwamba jinsi watu wanavyoifikiria na kuiona Torati itaamua nafasi yao mbinguni (ms. 19), na kwamba watu lazima waitii Torati vizuri zaidi kuliko waandishi na Mafarisayo, la sivyo hawataingia mbinguni (ms. 20).
Bila shaka, kitu alichokuwa anasema Yesu hapa ni watu kuishika Torati na kufanya kile kilichosemwa na Manabii. Angeitimiza Torati kwa maana kwamba Yeye angefunua kusudi la kweli la Mungu katika Torati Yake, akiifafanua kikamilifu, akikamilisha kile kilichokuwa kimekosekana katika ufahamu wa watu juu yake. Neno la Kiyunani linalotafsiriwa kutimiza katika mstari wa 17 ndilo linalotafsiriwa katika Agano Jipya sehemu nyingine na maana yake ni kukamilisha, kumaliza, kujaza na kutekeleza kabisa. Hayo ndiyo Yesu angefanya, akianzia sentensi kama nne hivi baadaye!
Hapana – Yesu hakuja kuondoa Torati bali kuitimiza, yaani, “kuijazia ikamilike.” Kwa habari ya zile amri zipatikanazo katika Torati na Manabii, Yesu aliweka wazi kabisa alichosema. Alitazamia kila mtu atii. Yote yaliyokuwemo yalikuwa muhimu kabisa. Ni hivi: Jinsi mtu anavyozistahi amri itaamua jinsi na yeye atakavyostahiwa mbinguni: “Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni” (5:19).
Tunafika kwenye mstari wa 20: “Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.”
Ona kwamba hilo si wazo jipya: ni la kumalizia ambalo lina uhusiano na ile mistari mingine yote kwa neno lile dogo – maana. Je, kushika amri ni muhimu kiasi gani? Ni lazima mtu azishike vizuri zaidi kuliko waandishi na Mafarisayo ili aweze kuingia katika ufalme wa mbinguni! Hapo tena tunaona kwamba haya ni mahubiri juu ya wokovu na utakatifu, na jinsi vinavyohusiana.
Je, Yesu Alikuwa Anazungumzia Haki Ya Namna Gani?
Yesu aliposema kwamba haki yetu lazima izidi ya waandishi na Mafarisayo, hakuwa anasema juu ya haki ile ya kisheria ambayo tungehesabiwa kama zawadi itolewayo bure? Hapana, kwa sababu mbili.
Kwanza: Mantiki haikubaliani na tafsiri hiyo. Kabla na baada ya kusema hivyo, Yesu alikuwa anazungumzia kuzishika amri, yaani, kuishi kwa haki. Tafsiri rahisi kabisa ya maneno Yake ni kwamba lazima tuishi kwa haki zaidi kuliko waandishi na Mafarisayo.
Pili: Ikiwa Yesu alikuwa anazunguma kuhusu haki tunayohesabiwa kisheria na kuipokea kama zawadi itolewayo bure kwa kumwamini, mbona hakutoa hata kidokezo? Mbona akasema kitu ambacho kingeweza kueleweka vibaya kirahisi tu na wale wakulima waliokuwa hawana elimu waliomsikiliza ambao wasingeweza kukisia kwamba alikuwa anazungumza nao juu ya haki ambayo tunahesabiwa na Mungu?
Tatizo letu ni kwamba hatutaki kukubali maana iliyo dhahiri ya mstari wenyewe, kwa sababu kwetu inasikika kama ni kutawaliwa na sheria. Lakini tatizo halisi ni kwamba hatuelewi muunganiko ulioko kati ya haki ya kuhesabiwa na haki halisi ya kivitendo. Mtume Yohana yeye alielewa, maana aliandika hivi: “Watoto wadogo, mtu na asiwadanganye; atendaye haki yuna haki, kama yeye alivyo na haki” (1Yohana 3:7). Wala hatuelewi mlingano kati ya kuzaliwa upya na haki ya matendo kama Yohana alivyoelewa. Anasema hivi: “Kila atendaye haki amezaliwa na yeye” (1Yohana 2:29).
Yesu angeweza kuongezea haya yafuatayo katika tamko Lake la Mathayo 5:20 – “Na kama mkitubu na kuzaliwa kweli mara ya pili na kupokea zawadi yangu itolewayo bure ya haki ipatikanayo kwa imani, haki yenu ya matendo itazidi ile ya waandishi na Mafarisayo kwa uwezo wa Roho wangu anayekaa ndani yenu.”
Haki Ya Waandishi Na Mafarisayo
Swali lingine ambalo ni muhimu, linalotokana na tamko la Yesu katika 5:20 ni hili: Je, waandishi na Mafarisayo walikuwa na haki kiasi gani (kimatendo)?
Kuna wakati mwingine ambapo Yesu aliwaita “makaburi yaliyopakwa chokaa ambayo kwa nje yanapendeza lakini ndani yamejaa mifupa ya wafu na uchafu wote” (Mathayo 23:27). Yaani, kwa nje walionekana ni wenye haki, lakini kwa ndani walikuwa waovu. Walifanya vizuri sana katika kushika Torati kama ilivyosema, lakini walipuuzia kusudi au maana yake, wakijitetea mara nyingi kwa kupindua kidogo au hata kubadilisha maagizo ya Mungu.
Hilo liliwekwa wazi na Yesu katika sehemu iliyofuata ya Mahubiri ya Mlimani. Alitaja amri kadhaa za Mungu, kisha akaonyesha tofauti kati ya kutimiza sheria na kutimiza kusudi au maana yake. Yesu alionyesha jinsi ambavyo waandishi na Mafarisayo walitafsiri na kutii kwa nje kila amri, kisha akafunua kusudi la kweli la Mungu kwa kila amri. Alianza kila mfano: “Mmesikia,” kisha akaeleza maoni ya Mungu kuhusu kile walichokuwa wamesikia. Anatumia amri ya sita kama mfano Wake wa kwanza.
“Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, ‘Usiue, na mtu akiua, itampasa hukumu.’ Bali mimi nawaambieni, ‘Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanamu ya moto. Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshtaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshtaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho’.” (Mathayo 5:21-26).
Waandishi na Mafarisayo walijivuna sana kwamba hawakuwa wauaji. Yaani, hawakuwahi kumwua mtu yeyote. Kwa mawazo yao, walikuwa wanaishika kabisa amri ya sita. Lakini, wangependa kumwua mtu kama isingekatazwa, kama inavyodhihirishwa kwa ukweli kwamba walifanya kila kitu kingine isipokuwa kuwaua waliowachukia. Yesu aliorodhesha mifano michache ya tabia yao ya kuua. Kutoka vinywani mwao walisema maneno mabaya ya matusi kwa wale waliokuwa wamewakasirisha. Kwa ndani walikuwa na uchungu, hawakusamehe, na wasiotaka mapatano, waliojitia katika kesi, ama kushtaki wengine au kushtakiwa kwa matendo yao ya kufisha na ya kichoyo. Waandishi na Mafarisayo walikuwa wauaji moyoni ambao walijizuia tu wasifanye kitendo chenyewe.
Lakini, yule ambaye ni mwenye haki wa kweli ni tofauti. Kiwango chake ni cha juu zaidi. Anajua kwamba Mungu anamtazamia ampende ndugu yake, na kama mahusiano yake na ndugu yake si mazuri, mahusiano yake na Mungu si sawa. Hatafanya matendo ya dini kinafiki, akijifanya kumpenda Mungu na huku anamchukia ndugu (ona Mathayo 5:23-24). Kama ambavyo Mtume Yohana angeandika baadaye, “Yeye asiyempenda ndugu yake ambaye anamwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hajamwona” (1Yohana 4:20).
Waandishi na Mafarisayo walifikiri kwamba wao walipata hatia kwa tendo la kuua tu. Lakini Yesu alionya kwamba hali ya moyo ya muuaji humfanya mtu kustahili jehanamu. Je, ni wangapi wanaojiita Wakristo ambao hawana tofauti na wale waandishi na Mafarisayo? Wamejaa chuki badala ya upendo. Wakristo wa kweli wamebarikiwa na Mungu mpaka kiwango cha Yeye kuweka pendo Lake ndani yao, akiwafanya wenye kupenda (ona Warumi 5:5) watu wote kwa neema Yake.
Mungu Anavyofafanua Uzinzi
Amri ya saba ikawa mfano wa pili wa Yesu kuhusu jinsi waandishi na Mafarisayo walivyoshika sheria huku wakipuuza maana yake.
“Mmesikia kwamba imenenwa, ‘Usizini;’ lakini mimi nawaambia, ‘Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani amekwisha kuzini naye moyoni mwake. Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanamu. Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanamu’.” (Mathayo 5:27-30).
Kwanza: Ona tena kwamba mahubiri haya ni kuhusu wokovu na utakatifu, na jinsi hayo mawili yanavyohusiana. Yesu alionya kuhusu jehanamu, na kinachotakiwa ili mtu asiende huko.
Waandishi na Mafarisayo wasingeweza kuipuuza amri ya saba, kwa hiyo waliitii kwa nje kwa kubaki waaminifu kwa wake zao. Lakini walikuwa wanafanya mapenzi na wanawake wengine katika mawazo yao. Walikuwa wanawavua nguo kimawazo wale wanawake waliowaona sokoni. Moyoni walikuwa wazinzi, na hivyo walikuwa wanaiasi maana ya amri ya saba. Je, ni wangapi wanaojiita Wakristo wanaoweza kusema wao ni tofauti?
Mungu alikusudia watu Wake wawe safi kabisa katika mahusiano ya kimwili. Kama nilivyokwisha sema katika kitabu hiki huko mwanzoni, ni makosa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mke wa jirani yako, lakini pia, ni makosa kuota kwamba unafanya mapenzi naye.
Je, kuna waliojisikia hatia miongoni mwa wasikilizaji wa Yesu? Bila shaka. Wafanyeje? Watubu mara moja, kama Yesu alivyoagiza. Wale waliokuwa na tamaa walitakiwa kuacha kutamani, kwa sababu wale wanaotamani watakwenda jehanamu. Hivyo, walipaswa kulipa gharama yoyote ile ili kumaliza jambo hilo.
Bila shaka si sawa kufikiri kwamba Yesu alimaanisha watu wenye tamaa wang’oe kweli jicho lao au kukata mkono. Mtu mwenye tamaa atakayeng’oa jicho lake atabaki mwenye tamaa aliye chongo! Yesu alikuwa anasisitiza kwa lugha ya mfano umuhimu wa kuitii maana ya amri ya saba. Mustakabali wa mtu milele ulikuwa unategemea hicho.
Je, unajisikia hukumu? Basi, “kata” chochote kinachokufanya ujikwae. Kama ni televisheni ya kulipia, acha kulipia. Kama ni televisheni kawaida, itupilie mbali. Kama ni kitu unachoona ukienda mahali fulani, basi acha kwenda huko. Kama ni gazeti unaloletewa nyumbani, acha kulipokea. Kama uko kwenye mtandao, jiondoe! Hakuna hata kimoja katika hivyo kinachofaa kukupeleka jehanamu milele. Hakuna mtu atakayekuwa jehanamu atakayesema, “Sawa niko jehanamu, lakini nilifurahia sana zile sinema mbaya nilipokuwa duniani. Sijuti, japo nitateseka huku jehanamu milele kwa sababu ya hilo.”
Maoni Ya Mungu Kuhusu Talaka
Mfano unaofuata wa Yesu unafanana kidogo na ule uliopita, ambao pengine ndiyo sababu unafuata mara moja. Labda ni sawa ufikiriwe kama ni nyongeza au mafafanuzi zaidi kuliko mada mpya. Kwa sababu hii, tofauti na ile mifano mingine ya Yesu iliyoanza kwa kusema “Mmesikia”, sehemu hii fupi inaanza hivi: “Imenenwa pia.”
“Imenenwa pia, ‘Mtu akimwacha mkewe, na ampe hati ya talaka.’ Lakini mimi nawaambia, ‘Kila mtu amwachaye mkewe isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi; na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini’.” (Mathayo 5:31-32).
Huu ni mfano mwingine kuhusu jinsi waandishi na Mafarisayo walivyoishika sheria huku wakikataa maana yake.
Hebu tutengeneze Farisayo wa kufikirika tu, aliyeishi siku za Yesu. Ng’ambo ya pili ya mtaa alioishi kuna mwanamke mrembo ambaye anamtamani. Kila siku wakionana anamtania-tania. Mwanamke naye anaonekana kama anampenda, na tamaa yake inaongezeka. Angependa kumwona akiwa uchi, na mara nyingi anapofikiri anamwaza wakifanya mapenzi. Laiti angeweza tu kumpata!
Lakini ana tatizo. Yeye ana mke na yule mwanamke naye ana mume, na dini yake inakataza uzinzi. Hataki kuvunja amri ya saba (hata ingawa kila alipomtamani alikwisha ivunja). Je, afanye nini?
Kuna jibu! Kama wote wawili wakiachana na wenzi wao, anaweza kumwoa huyo mpenziwe! Lakini je, ni halali kupata talaka? Ndiyo! Kuna andiko kabisa! Kumbukumbu la Torati 24:1 inasema juu ya kumpa mkeo cheti cha talaka wakati unapompa talaka! Talaka inaruhusiwa katika mazingira maalum! Ni yapi hayo? Anasoma kwa makini kile Mungu alichosema.
Mtu akiisha kutwaa mke kwa kumwoa, asipopata kibali machoni mwake kwa kuwa ameona neno ovu kwake, na amwandikie hati ya kumwacha, akamtilie mkononi mwake, na kumtoa katika nyumba yake … (Kumbu. 24:1).
Aha! Anaweza kumpa mkewe talaka kama atagundua neno ovu kwake! Naye amekwisha gundua tayari! Havutii kama yule mwanamke wa mtaa wa pili!
Basi, anamwacha mke wake kihalali kabisa kwa kumpa hati ya kumwacha (na inapatikana katika ofisi ya Chama cha Mafarisayo), na kwa haraka anamwoa yule mwanamke aliyekuwa anamtaka, ambaye naye ameachika kihalali. Na hayo yanatokea bila ya kujisikia hatia hata kidogo kwa sababu Torati ya Mungu imefuatwa.
Lakini kwa kweli, Mungu anaona mambo kitofauti. “Neno ovu” linalotajwa hapo kwamba ni ruhusa ya talaka, ni kama Yesu alivyosema, “uasherati”. Yaani, mume alikuwa na ruhusa ya kumwacha mke wake kama angegundua kwamba hakuwa mwaminifu kabla ya ndoa yao (yaani, wakati wa uchumba) au wakati wakiwa na ndoa. Na Yesu mahali pengine alikuwa amesema kwamba, sababu ya pekee iliyoruhusu talaka katika mazingira hayo ilikuwa ni “ugumu wa mioyo” yao (Mathayo 19:8). Yaani, mume mwenye moyo mzuri angemsamehe mwanamke ambaye hakuwa mwaminifu ambaye angetubu. (Mke asiyetubu ni jambo lingine hilo.)
Katika mtazamo wa Mungu, huyo mwanamume wa kufikirika tuliyemsema sasa hivi hana tofauti yoyote na mwasherati. Ameivunja amri ya saba. Ukweli ni kwamba ana hatia kuliko hata yule mwasherati wa kawaida, maana yeye ni “mwasherati mara mbili”. Kwa vipi? Kwanza: Yeye mwenyewe amezini. Yesu alisema baadaye kwamba, “Yeyote amwachaye mke wake, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, akamwoa mwingine, azini” (Mathayo 19:9).
Pili: Kwa sababu, huyo mkewe aliyeachika sasa lazima atafute mume mwingine ili aendelee kuishi. Basi, katika mtazamo wa Mungu, huyo Farisayo amefanya kitendo kinacholingana na kumlazimisha mke wake awe na uhusiano wa kimwili na mwanamume mwingine. Sasa, anakuwa na hatia kwa “uasherati” wa mkewe. Yesu alisema hivi, “Kila amwachaye mke wake, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, amfanya azini” (Mathayo 5:32 – Maneno mepesi ili kutilia mkazo).
Yawezekana kwamba Yesu hata alimhukumu huyo Farisayo wetu mwenye tamaa kwa kosa la “uasherati mara tatu” ikiwa tamko Lake kwamba, “na kila amwoaye mwanamke aliyeachwa azini” (Mathayo 5:32) linamaanisha kwamba Mungu anamhesabu huyo Farisayo kuwa na hatia kwa sababu ya “uasherati” wa mume mpya wa mke wake wa zamani.
Hili lilikuwa swala kubwa katika siku za Yesu, kama tunavyosoma mahali pengine ambapo Mafarisayo fulani walimwliza hivi: “Je, ni halali kwa mwanamume kumwache mke wake kwa sababu yoyote?” (Mathayo 19:3). Swali lao linadhihirisha mioyo yao. Bila shaka baadhi yao walitaka kuamini kwamba sababu yoyote inafaa kwa talaka kutolewa.
Lazima niongeze kwamba ni aibu sana wakati Wakristo wanapochukua mistari hiyo hiyo kuhusu talaka, kuitafsiri vibaya, kisha kuweka vifungo vizito juu ya watoto wa Mungu. Yesu hakuwa anazungumza juu ya Mkristo ambaye aliachana na mwenzake wakati wote wakiwa wenye dhambi, na ambaye baada ya kumpata mwenzi mzuri tu anayempenda Kristo, wanaoana. Huo si uasherati hata kidogo! Na kama hayo ndiyo Yesu alikuwa anazungumzia, basi itabidi tubadilishe Injili, kwa sababu haitoi tena msamaha kwa dhambi zote za wenye dhambi. Tangu sasa itabidi tuhubiri hivi: “Yesu alikufa kwa ajili yako, na ukitubu na kumwamini, utasamehewa dhambi zako zote. Lakini, kama una talaka, hakikisha kwamba huingii tena katika ndoa maana utakuwa mwasherati, na Biblia inasema waasherati wote watakwenda jehanamu. Tena, kama uliachana na mwenzi kisha ukawa na ndoa tena, kabla ya kuja kwa Kristo itakubidi utende dhambi nyingine moja na kuachana na mwenzako mliye naye sasa. Vinginevyo utaendelea kuishi katika uasherati, na waasherati hawajaokoka.” Je, hiyo ndiyo Injili?
Kuhusu Kuwa Wakweli
Mfano wa tatu wa Yesu kuhusu tabia isiyo haki na kutafsiri vibaya maandiko kulikofanywa na waandishi na Mafarisayo unahusu amri ya Mungu kusema ukweli. Waandishi na Mafarisayo walikuwa wametunga njia ya kijanja sana ya kudanganya. Tunajifunza kutoka Mathayo 23:16-22 kwamba waliamini hawakuwajibika kutunza viapo vyao kama waliapa kwa hekalu, madhabahu au mbingu. Lakini kama wangeapa kwa dhahabu ya hekaluni, au sadaka iliyokuwa madhabahuni, au kwa Mungu wa mbinguni, basi walitakiwa kutimiza viapo vyao!
Huu unafiki ndiyo ukawa mada iliyofuata katika mahubiri maarufu ya Yesu.
“Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, ‘Usiape uongo, ila mtimizie Bwana nyapo zako.’ Lakini mimi nawaambia, ‘Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu’.” (Mathayo 5:33-37).
Amri ya Mungu kuhusu viapo haikusema chochote juu ya kufanya viapo kwa kuvijenga juu ya kitu chochote. Mungu alikusudia watu Wake wawe waaminifu kutunza maneno yao. Wakati watu wanapolazimika kutumia kiapo ili kuwafanya wengine waamini maneno yao, huo ni ukiri wa dhati kwamba wakati mwingine huwa wanadanganya. Neno letu linapaswa kuwa kama lilivyo, bila kuhitaji viapo. Je, haki yako inazidi ya waandishi na Mafarisayo katika eneo hilo?
Dhambi Ya Kulipiza Kisasi
Kinachofuata kwenye orodha ya Yesu ni kupotoshwa kwa mstari maarufu sana katika Agano la Kale kulikofanywa na Mafarisayo.
“Mmesikia kwamba imenenwa, ‘Jicho kwa jicho, na jino kwa jino.’ Lakini mimi nawaambia, ‘Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili. Akuombaye mpe; naye atakaye kukopa kwako, usimpe kisogo’.” (Mathayo 5:38-42).
Torati ya Musa ilitangaza kwamba kama mtu angepatikana na hatia katika baraza, ya kumjeruhi mtu mwingine, adhabu yake ingekuwa sawa na madhara aliyosababisha. Kama alimtoa mtu jino, yeye naye la kwake litolewe, kwa haki kabisa. Hii amri iliwekwa ili kuhakikisha kwamba haki ilikuwepo barazani kwa ajili ya makosa makubwa. Lakini tena, waandishi na Mafarisayo waliigeuza, wakaifanya kuwa amri nyingine kabisa iliyofanya kisasi kuwa wajibu mtakatifu! Inaonekana walikuwa hawana suluhu, wakitafuta kulipiza kisasi hata kwa kosa dogo kabisa.
Mungu mara zote anatazamia ziada kutoka kwa watu Wake. Kulipiza kisasi ni kitu anachokataza kabisa (ona Kumbu. 32:35). Agano la Kale lilifundisha kwamba watu wa Mungu waonyeshe wema kwa adui zao (ona Kutoka 23:4-5; Mithali 25:21-22). Yesu aliunga mkono kweli hiyo kwa kutuambia tugeuze shavu la pili na kwenda maili ya zaidi tunaposhughulika na watu waovu. Tunapokosewa, Mungu anataka tuwe na huruma, tukilipa jema mahali tulipofanyiwa uovu.
Lakini je, Yesu anatazamia kweli tuwaruhusu watu wengine watuonee na kututumia, mpaka kuwaruhusu waharibu maisha yetu kama ndicho wanachotaka? Je, ni makosa kumpeleka asiyeamini mahakamani, kutafuta haki kwa tendo lisilo halali ambalo tumetendewa? Hapana. Yesu hakuwa anazungumza juu ya kupata haki kwa ajili ya makosa makubwa mahakamani, bali alizungumza juu ya kujilipiza kisasi kibinafsi kwa ajili ya makosa madogo madogo. Ona kwamba hakusema tutoe shingo zetu ili tunyongwe na yule ambaye ametuchoma kisu mgongoni. Hakusema kwamba mtu akidai gari letu, tumpe na nyumba. Yesu alikuwa anatwambia jinsi ya kuonyesha uvumilivu na huruma kwa kiwango cha juu sana wakati tunapokabiliana na makosa madogo madogo na changamoto za kawaida za kushughulika na watu wenye ubinafsi. Hatazamii twende “maili mia zaidi”, anatazamia twende “maili moja zaidi”. Anataka tuwe wema kuliko watu wabinafsi wanavyotazamia, na tusiwe wachoyo na fedha zetu, tukitoa kwa ukarimu na kukopesha. Waandishi na Mafarisayo hawakufika hata nusu ya kiwango hicho. Vipi wewe – haki yako inazidi yao katika eneo hili?
Siwezi kuacha kuuliza hivi: Mbona wengi wanaojiita Wakristo wanakwazwa kirahisi mno? Mbona wanakasirishwa upesi na vikwazo ambavyo ni vidogo mara kumi kuliko kupigwa kofi shavuni? Je, watu hao wameokoka?
Kuwapenda Jirani Zetu
Mwisho Yesu akataja amri nyingine moja iliyotolewa na Mungu ambayo waandishi na Mafarisayo walikuwa wameibadilisha ili kulingana na mioyo yao yenye chuki.
“Mmesikia kwamba imenenwa, ‘Umpende jirani yako’ na ‘Umchukie adui yako’. Lakini mimi nawaambia, ‘Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni. Maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo? Basi, ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu’.” (Mathayo 5:43-48).
Katika Agano la Kale, Mungu alikuwa amesema hivi: “Mpende jirani yako” (Walawi 19:18), lakini waandishi na Mafarisayo, kwa mawazo yao tu, wakawa wamefikiri kwamba, kama Mungu alitaka wawapende jirani zao, basi pia alimaanisha wawachukie adui zao. Ukawa wajibu wao mtakatifu. Lakini, kulingana na Yesu, Mungu hakumaanisha hivyo, na wala hakusema hivyo.
Baadaye Yesu angefundisha katika hadithi ya Msamaria Mwema kwamba tunapaswa kumhesabu kila mtu kuwa ni jirani yetu. Mungu anataka sisi tumpende kila mtu, pamoja na adui zetu. Hicho ndicho kiwango cha Mungu kwa watoto Wake, ambacho Yeye Mwenyewe anakifuata. Yeye hutuma mvua na jua kwa ajili ya kukuza mazao, si kwa watu wema tu, bali hata kwa waovu. Tunapaswa kufuata mfano Wake, tukionyesha wema kwa watu hata wasiostahili. Tukifanya hivyo, tunaonyesha kwamba sisi ni “wana wa Baba [yetu] aliye mbinguni” (Mathayo 5:45). Watu waliozaliwa upya kweli kweli hutenda kama Baba yao.
Upendo ambao Mungu anatazamia tuwaonyeshe adui zetu si hisia au kukubaliana na uovu. Mungu hatulazimishi tuwe na hisia za joto zisizoeleweka kuhusu wanaotupinga. Hatuambii tuseme kisichokuwa kweli, kwamba adui zetu ni watu wazuri kweli. Lakini anatutazamia tuwapende na kuchukua hatua za makusudi kuonyesha hilo, haidhuru basi iwe ni kwa kuwasalimu vizuri na kuwaombea.
Vipi Wewe?
Mpaka hapa unatambua kwamba waandishi na Mafarisayo hawakuwa wenye haki hata kidogo. Walikuwa na aina fulani ya haki ya nje, lakini, sawa tu na wengi wanaojiita Wakristo, walikuwa wenye chuki, tamaa mbaya, wabinafsi, wenye kulipiza kisasi, wasio na huruma, wachoyo, na wadanganyifu wenye kubadili Maandiko. Lakini, kulingana na Yesu, waamini wa kweli wanaonyeshwa kuwa wapole, wenye njaa ya haki, wenye rehema, wasafi moyoni, wapatanishi na wanaoudhiwa au kuteswa. Basi, sehemu hii ya Mahubiri ya Mlimani inatakiwa ifanye mambo mawili: Aidha ikujaze uhakika kwamba kweli wewe umezaliwa mara ya pili, au ikujaze hofu kwa sababu unatambua kwamba huna tofauti na wale waliohukumiwa na kulaumiwa na Yesu. Kama uko katika fungu la kwanza, wewe kama wengine wote hapo tambua kwamba bado una nafasi ya kufanya maboresho. Lakini, ukamilifu ndilo lengo lako kwa sababu ndilo lengo la Mungu kwa ajili yako, kama alivyosema Yesu (ona Mathayo 5:48; ona pia Wafilipi 3:12-14).
Kama uko kwenye lile fungu la pili, unaweza kutubu na kuwa mtumwa wa Yesu kwa kumwamini. Mara moja utajisikia ukihamishwa na Mungu na kuingizwa katika fungu lile la kwanza kwa neema Yake!
Yaliyomo | Sura Iliyopita | Sura Ifuatayo | Mwanzo wa Ukurasa | Pa Kuanzia
|